TAMIDA YAIPONGEZA KAMPUNI YA SAB GOLD,UFADHILI OFISI DAR

 TAMIDA YAIPONGEZA KAMPUNI YA SAB GOLD,UFADHILI OFISI DAR

Makamu Mwenyekiti wa Chama cha Wanunuzi na Wauzaji wa Madini Tanzania (TAMIDA) ambaye pia Mkurugenzi Mtendaji wa GEM TANZANITE LTD akizungumza na wanahabari [hawapo pichani]jijini Dar es Salaam 

Na Thadei Praygod,Dar Es Salaam

Chama cha Wanunuzi wa Wauzaji wa Madini Tanzania [TAMIDA]kimepongeza hatua ya Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam,Amos Makalla kutembelea soko la madini la mkoa huo na kuzindua ofisi za chama hicho.

Akitoa pongezi hizo mbele ya waandishi wa Habari jijini humo Makamu Mwenyekiti  wa Chama hicho ambaye pia ni mkurugenzi wa kampuni ya Gem Tanzanite Limited, Osman Tharia alisema  wanaIpongeza hatua ya Serikali katika kukendelea kukuza sekta ya madini ambapo pia alisema uwepo wa ofisi rasmi za Tamida ni hatua itakayowainua wauzaji,wanunuaji  wa madini wadogo,wa kati na hata wakubwa.

Alisema kuwa wanaipongeza hatua ya mkuu wa mkoa huo Amos Makalla ya kuahidi kutoa ushirikiano mkubwa kwa soko la madini la Dar es Salaam sambamba na kuboresha mazingira ya soko hilo ili yaendane na masoko mengine ya madini duniani.

Alisema uzinduzi wa ofisi za  [TAMIDA]ambazo zimefadhiliwa na kampuni ya Sab Gold LTD ni mwendelezo wa kampuni hiyo kuendelea kusaidia wafanyabiashara wa madini hasa ya dhahabu kupitia chama cha wanunuzi na wauzaji wa madini Tanzania.

 ''Sisi kama chama cha wanunuzi na wauzaji wa madini Tanzania [TAMIDA]tunaishukuru sana kampuni ya Sab Gold Limited [SGL] kwa kutufadhili katika ofisi hii ambayo lengo letu ni kutoa ushauri kwa wachimbaji,wauzaji na wanunuzi wa madini na kuwaunganisha na wafanyabiashara wengine kwa kuwatafutia masoko ya uhakika ya madini''alisema Bw Tharia .

Aidha Tharia aliongeza kuwa kupitia ufadhili wa kampuni ya Sab Gold  Limited ambayo ina malengo makubwa kwa wachimbaji wa madini ya dhahabu hapa nchini ikiwemo ununuzi wa dhahabu kwa bei nzuri,chama cha wauzaji na wanunuzi wa madini Tanzania kitaendelea kuwasaidia wachimbaji wadogo wa madini huku akiwasisitiza wafanyabiashara wa mnadini kujiunga na chama hicho ili kwa pamoja waendeleze soko la madini.

Kuhusu faida za kujiunga na TAMIDA  Bw Tharia alisema kuwa wafanyabiashara wadogo,wa kati na wakubwa ,madalali wa madini[brokers] pamoja na wachimbaji wa madini hasa hasa dhahabu watafaidika kwa kupatiwa elimu ya madini,kuunganishwa na masoko pamoja na kupatiwa ushauri wa namna ya kuchimba,kuandaa  na kuuza madini hayo.

Mkuu wa mkoa wa Dar es Salaam,Amos Makala alitembelea soko la madini la Dar es Salaam na kuzindua ofisi za TAMIDA oktoba 25 mwaka huu.

 

Comments