UDSM chaadhimisha Kilele cha Miaka 60, chatoa msaada Kituo Afya Kimara

 UDSM chaadhimisha Kilele cha Miaka 60, chatoa msaada Kituo Afya Kimara




 
 Dar es Salaam

Katika kuadhimisha Kilele cha Miaka 60 ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) tangu kuanzishwa kwake Oktoba 25 mwaka 1961, chuo hicho  kimetoa msaada wa vitakasa mikono, viti vya kuhudumia wagonjwa (Viti Maguru) pamoja na mashuka katika Kituo cha Afya Kimara kilichopo Wilayani Ubungo, Dar es Salaam.

Akizungumza katika hafla ya kukabidhi vifaa hivyo Makamu Mkuu wa Chuo hicho,  Profesa William Anangisye amesema maadhimisho hayo yatakuwa endelevu kwa mwaka wote wa masomo kwa kutoa vifaa mbalimbali kwa vituo vya Afya kuanzia Oktoba 25 mwaka huu.

Amebainisha kuwa UDSM kinazidi kukuua na idadi ya wanafunzi kuongezeka ambapo kwa sasa kina zaidi ya wanafunzi 43,307 wanawake zaidi ya19,784 na kwamba kila mwaka wanapokea idadi kubwa ya maombi ya wanafunzi wanaotamani kujiunga zaidi ya mara mbili ya uhitaji wa chuo.

Amesisitiza kuwa chuo hicho kimeweka mikakati, malengo, mipango na hatua tofauti kufikia ikiwemo ni pamoja na kuongezeka kwa duru ya za mahafali ya mwisho wa mwaka kuanzia mwaka 2021 kuboresha matokeo ya tafiti pamoja na ubunifu kutoka vyanzo vya ndani, ujenzi wa maabara na miundombinu ya kusomea.

" UDSM kitaendelea na maadhimisho haya kwa mwaka mzima kuanzia tar 25 oktoba 2021 kwa kutoa vifaa mbalimbali vya kiafya na kielimu kwa taasisi mbalimbali, shule na hospitali," amesema Profesa Anangisye.

Ameongeza kuwa wanajipanga kutoa msaada wa vifaa vya kufundishia, maarifa ya ufundishaji katika Shule ya Mahitaji Maalum Sinza na kwamba bado kinaendelea utoaji wa elimu ya Ujasiriamali kwa wahitimu.

Amefafanua kuwa chuo hicho kitafanya makongamano ya kitaifa yenye lengo la kuleta tija kwa taifa na kwamba kinawakaribisha watunga sera, wadau wa maendeleo, asasi za kiraia kushiriki katika maadhimisho hayo.

Naibu Makamu Mkuu wa UDSM anayeshughulikia Utafiti na Huduma kwa Jamii, Profesa Bernadeta Killian amesema katika kuadhimisha kilele hicho wametoa msaada wa mashuka 100, viti maguru vinne pamoja na vitakasa mikono 60 katika kituo hicho na kwamba wanajipanga kwenda kuisaidia shule hiyo.   

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Halmashauri ya Manispaa ya Ubungo, Beatrice Dominic amekishukuru chuo hicho kwa msaada huo kwani utawasaidia kwa kiasi kikubwa wahitaji na kujaza nafasi ambazo zilikuwa zinahitaji

Mkurugenzi huyo amesema kwa siku kituo hicho kinahudumia watu wengi hivyo mahitaji ni makubwa kuliko eneo linavyoonekana na kutokana na ufinyu wa eneo ilibidi kijengwe kwa ramani tofauti na vituo vingine

Amekihakikishia chuo hicho kuwa  vifaa hivyo vitatunzwa kwa umakini ili viendelee kutoa huduma iliyokusudiwa pamoja na kubaki katika ubora wake.

Aidha, amesema bado manispaa hiyo inatoa fedha za mapato yake ya ndani kwa ajili ya upanuzi wake na wanasaidiwa pia na Wakala wa Barabara Nchini (TANROADS) na TAMISEMI na kikikamilika watahudumia watu wengi zaidi na kuboresha huduma ya afya kwa jamii.

Nae, Mganga Mfawidhi wa Kituo hicho, Dickson Masele amekipongeza UDSM kwa kuadhimisha miaka 60 na kukishukuru kwa msaada wa vifaa hivyo huku akikihakishia chuo hicho kuvitunza vifaa hivyo kwa umakini wa hali ya juu.

Comments