WATAKAOHAMIA MAGOMENI KOTA WATAKIWA KUZITUNZA NYUMBA HIZO.

 WATAKAOHAMIA MAGOMENI KOTA WATAKIWA KUZITUNZA NYUMBA HIZO.



Na Praygod THADEI,

Dar es salaam

Wakaazi 645 waliokuwa wakiishi katika nyumba za Magomeni kota kabla ya kuhamishwa na wanaotarajia kuhamia katika majengo mapya yaliyojengwa na wakala wa majengo TBA wametakiwa kuzitunza nyumba hizo pindi watakapokabidhiwa.

Wito huo umetolewa na katibu mkuu wizara ya ujenzi na uchukuzi  Mhandisi Balozi Aisha Amour wakati alipotembelea mradi huo wa nyumba hizo zilizojengwa katika eneo la magomeni Kota wilayani Kinondoni jijini Dar es salaam ambapo amesisitiza kuwa endapo nyumba hizo zitatunzwa vyema hali hiyo itasaidia kudumu kwa nyumba hizo miaka na miaka.

Aidha ameongeza kuwa wananachi hao ambao wataishi katika nyumba hzio bila malipo kwa muda wa miaka mitano na baadaye kuzipangisha ama kuzinunua kwa bei nafuu watakabidhiwa nyumba hizo wakati wowote kuanzia sasa.

Kuhusu hatua zilipofikia hatua za ujenzi wa nyumba hizo Mhandisi,Balozi Amour amesema ameridhishwa na kasi yake huku akiwataka wakala wa majengo TBA kuharakisha ili wananchi waweze kuhamia.

Kwa upande wake Mtendaji mkuu  wa wakala wa majengo nchini TBA ,Arch Daud Kondoro amesema tayari nyumba zimekamilika baada ya kumalizia kuziwekea umeme pamoja na lifti  na wakazi wote 645 watakabidhiwa nyumba hizo baada ya kukamilika kwa taratibu za uhakiki huku akiwaondoa shaka wakaazi hao kuhusu kuhamia katika nyumba hizo za kisasa.

Ameongeza kuwa katika mradi huo wa nyumba hizo pia wameweka vizimba vya biashara zaidi ya 186 pamoja na vyoo vya kisasa vya  kulipia .

Comments