Skip to main content

WAZIRI MKUU: WATANZANIA TUJIVUNIE UVUMBUZI WA MBEGU MPYA YA MICHIKICHI

 

WAZIRI MKUU: WATANZANIA TUJIVUNIE UVUMBUZI WA MBEGU MPYA YA MICHIKICHI


NA MWANDISHI WETU
 
WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amesema Watanzania wana kila sababu ya kutembea kifua mbele na kujivunia utafiti uliofanyika hapa nchini na kupata mbegu mpya ya michikichi ambayo imeonesha mafanikio makubwa.

“Baada ya kukaa na kufanya tathmini ya zao la chikichi hapa Tanzania, na leo nimesikia michango ya wadau wote. Nimejiridhisha kwamba utafiti tulioufanya wa kuzalisha mbegu ya Tanzania ambayo inaota na kutoa matunda ndani ya miaka miwili hadi mitatu, ninayo furaha kutamka kuwa utafiti ule umefanikiwa,” alisema na kuamsha shangwe miongoni mwa wadau wa zao hilo.

Waziri Mkuu ametoa kauli hiyo jana usiku (Jumapili, Februari 26, 2023) wakati akihitimisha kikao chake na wadau wa zao la chikichi mkoani Kigoma kwenye ukumbi wa NSSF. Mbegu hiyo bora ya michikichi aina ya TENERA inatoa mafuta mara tatu zaidi ya aina ya DURA ambayo inalimwa na wakulima kwa takribani asilimia 90.

Alisema mtu yeyote anayetaka kulima chikichi anaweza kufanya hivyo kwa sababu mbegu zipo. “Tulianza kuzalisha mbegu mwaka 2018 na ilipofika mwaka 2020 tukaanza kupanda miche na leo tunaona matunda yanapatikana.”

“Twendeni mashambani, tutumie miche yetu iliyozalishwa ama na taasisi zetu, Halmashauri zetu au vyama vya msingi (AMCOS). Tuna kazi ya kuhakikisha zao la chikichi linaenda kwa spidi kali zaidi.” 

“Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ametuagiza kila mkoa, kila wilaya tutenge maeneo ya kilimo lakini kuna baadhi hadi leo hii bado hamjagawa maeneo, tena vijana wapo na wanataka kulima. Inasikitisha kuona wataalamu tupo, nia ya dhati ya Serikali ipo lakini watu hamchukui maamuzi. Tunataka sasa, tutoke hapo tulipo.”

Akifafanua kuhusu umuhimu wa kuwa na mashamba makubwa ya michikichi, Waziri Mkuu alisema si lazima mashamba hayo yalimwe au kumilikiwa na mtu mmoja. “Jiungeni watu kadhaa na mtenganishe hizo ekari zenu kwa barabara lakini lazima yawe sehemu moja,” alisisitiza.

Akitoa maagizo mahsusi kabla ya kufunga kikao hicho, Waziri Mkuu alizitaka Halmashauri zinazolima zao la chikichi, ziimarishe vitalu vya miche ya zao hilo. Pia alizitaka zitoe fedha zilizokuwa zinatengwa kwa ajili ya vitalu na kuzipatia taasisi zinazozalisha miche ikiwemo TARI–Kihinga, JKT Bulombora na gereza la Kwitanga ili zizalishe miche kwa ajili ya Halmashauri husika na kisha wazisambaze bure kwa wakulima katika maeneo yao.

Comments