POLISI KUENDELEA KUTUMIA TEHAMA KUPAMBANA NA UHALIFU

 

                                    *******

Na Abel Paul wa Jeshi la Polisi- Dar es salaam

Jeshi la Polisi limesema litaendelea kutumia Tehama na mifumo katika kupambana na uhalifu wa kimtandao hapa Nchini,kutokana na Mabadiliko ya sayansi na Teknolojia na Ulimwengu wa sasa ambao wahalifu wamekuwa wakiutumia kutenda uhalifu.

Hayo ameyasema leo Agosti 17,2023 na Mkuu wa chuo cha Taaluma ya Polisi Dar es salaam (DPA) Kamishna msaidizi Mwandamizi wa Polisi SACP Dkt Lazaro Mambosasa wakati akipokea Kompyuta kutoka kwa kampuni ya Sura Technologies  Company Limited ya Jijini Dar es salaam ambapo amebainisha kuwa kompyuta hizo zitasaidia katika ufundishaji kwa askari walioko katika mafunzo.

Daktari Mambosasa amebainisha kuwa kompyuta hizo ni za kisasa ambazo zitawasaidia wakufunzi katika kufundisha wanafunzi waliopo katika chuo cha Taaluma ya Polisi Dar es salaam (DPA) huku akitoa rai kwa wanafunzi kutumia vifaa hivyo vizuri ili viwanufanishe katika kupata mafunzo ya Tehama ambayo ndio dira ya Dunia kwa sasa.

Kwa upande wake Bwana Edmund Mbao kutoka Sura Technologies Company Limited amesema kuwa wao kama wadau wa kupinga maswala ya kihalifu waliona ni vyema watoe vifaa hivyo vya Tehama kwa Jeshi la Polisi ambalo linahusika moja kwa moja na mapambano ya uhalifu hapa Nchini ambapo amebainisha kuwa wanaamini vifaa hivyo vinakwenda kutumika katika kufundisha askari ambao watapata mafunzo ya Tehama ili kukabiliana na uhalifu wa kimtandao hapa Nchini.

Nae Mkufunzi Mkuu wa chuo cha Taaluma ya Polisi Dar es salaam Kamishna msadizi wa Polisi ACP Andrea Legembo amesema kuwa kompyuta hizo zitakwenda kuongeza ufanisi wa ufundishaji wa Tehama kwa wanafunzi na wakufunzi wa chuo cha Taaluma ya Polisi Dar es salaam (DPA).


Comments