Skip to main content

JUMIKITA YAWASHUKURU WATANZANIA KUUNGA MKONO KAMPENI KUPINGA UDHALILISHAJI DHIDI YA MTOTO WA KIKE

 

JUMIKITA YAWASHUKURU WATANZANIA KUUNGA MKONO KAMPENI KUPINGA UDHALILISHAJI DHIDI YA MTOTO WA KIKE



Mwenyekiti wa Jumuiya ya Wanahabari wa Mitandao ya Kijamii Tanzania (JUMIKITA) Shaaban Matwebe akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam.

NA MWANDISHI WETU

MWENYEKITI wa Jumuiya ya Wanahabari wa Mitandao ya Kijamii Tanzania (JUMIKITA) Shaaban Matwebe amesema kuwa Watanzania wamekuwa na mwitikio mkubwa wa kuunga mkono kampeni ya kupinga udhalilishaji wa wanawake katika mitandao ya kijamii.

Hivi karibuni  Matwebe aliyataka mashirika na Watetezi wa Haki za Wanawake kujitokeza na kukemea na kulaani vikali tabia mpya na mbaya inayotaka kujitokeza nchini ya kutukana matusi wanawake viongozi mitandaoni.

Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam Matwebe aamewashukuru Watanzania kwa mapokeo mazuri juu ya kampeni hiyo.

"Nawashukuru Watanzania kwasababu badala ya kutoa taarifa sasa tunatakiwa kuonyesha tunachukia, tunakataa na kukemea matusi mitandaoni, mapokeo yamekuwa ni mzauri," amesema Matwebe na kuongeza,

"Mpaka sasa watu wengi wamejitokeza kuunga mkono kampeni ya kukataa matusi mitandaoni, kampeni ya kukataa kumdhalilisha mtoto wa kike. Ili tufanikiwe kupinga vita hii ya udhalilishaji wa mtoto wa kike, niwaombe Watanzania kwamba kampeni inayoendeshwa ya kumshtaki au kutoa malalamiko Insta au Twitter kwa kila mtu mwenye ushawishi afanye hivyo ili tuweze kufanikiwa kwenye kampeni hii,".

Ametumia fursa hiyo kuomba kama ikiwezekana Serikali ya Marekani iunge mkono kampeni hiyo ya kumlinda mtoto wa kike, kwamba Serikali ya Marekani ikiwezekana itoe taarifa ya kuonyesha mambo inayoyaunga mkono na yale isiyoyaunga mkono.

Matwebe amemtaka kila mtu atumie kila njia anayoweza katika kufanikisha kampeni hiyo, na kwamba kila mtu aonyeshe kukataa na kukemea udhalilishaji wa utu wa mwanamke.

Akizungumza hivi karibuni Matwebe alisema tabia ya udhalilishaji wa mtoto wa kike mitandaoni ni mbaya na chafu yenye kulenga kudhalilisha na kutweza utu wa mtu bila kujali heshima, umri na nafasi yake katika jamii jambo ambalo halikuwahi kuwa utamaduni wa Watanzania.

"Pia kama jukwaa la wanahabari wa mitandao ya kijamii Tanzania (JUMIKITA) tunawataka mashirika na watetezi wa haki za wanawake kujitokeza katika hili," alisema Matwebe.

Matwebe aliyataja baadhi ya mashirika hayo kuwa ni Tanzania Gender Networking Programme (TGNP), Tanzania Women Lawyers Association (TAWLA), Tanzania Media Women's Association (TAMWA) na Umoja wa Wanawake wa Wanasiasa (WCP-Ulingo).

Hivyo alisema ni wakati sahihi wa kujitokeza hadharani na kusimamia masuala haya wakati mwanamke mwenzao anaposhambuliwa kwa kudhalishwa kwa matusi mazito ya nguoni kwa sababu ya jinsia yake.

Kadhalika aliliomba kundi la viongozi wa Dini pia lisikae kimya wala lisikae pembeni katika kukemea swala hili la matusi mitandaoni.

"Tunatoa wito kwa viongozi wa Dini kuongea na waumini wao kwa Dini zao na madhehebu yao kama sehemu ya kusimamia maadili ya waumini wao. Lakini pia tunaitaka erikali kutoa kauli ya kukemea hilo na kusimamia sheria za nchi dhidi ya utamaduni mpya na mbaya wa matusi kwa wananchi na viongozi wa nchi," aliongeza Matwebe na kusema,

"Tupige vita matusi mitandaoni, tukemee matusi mitandaoni na tuepuke matusi mitandaoni. Matusi hayana kabila, dini wala chama. Leo anatukanwa Mzazi wa mwenzio kesho atatukanwa mzazi wako,"

Comments