RAIS WA MSUMBIJI KUWASILI NCHINI KESHO,NDIYE MGENI RASMI UFUNGUZI MAONESHO YA SABASABA

 RAIS WA MSUMBIJI KUWASILI NCHINI KESHO,NDIYE MGENI RASMI UFUNGUZI MAONESHO YA SABASABA 


Waziri wa Mambo ya nje na ushirikiano wa Afrika Mashariki, January Makamba akizungumza na waandishi wa Habari (hawapo pichani) Jijini Dar Es Salaam juu ya ziara ya Rais wa Jamhuri ya watu wa Msumbiji,Filipe Nyusi ambaye atawasili nchini hapo Kesho.



Na Thadei PrayGod,Dar Es Salaam 

Rais wa Jamhuri ya  Msumbuji Mhe. Filipe Jacinto Nyusi anatarajiwa kufanya ziara ya kikazi ya takrinani siku nne hapa nchini itakayoangazia masuala mbalimbali ikiwemo Ufunguzi wa maonyesho ya kimataifa ya biashara maarufu kama Sabasaba.

Akizungumza na waandishi wa Habari mapema hii Leo Jijini Dar Es Salaam,Waziri wa Mambo ya nje na ushirikiano wa Afrika Mashariki Mhe January Makamba (Mb) amesema kwamba ziara ya Rais huyo kuitembelea Tanzania inafanyika Kwa mwaliko maalum aliyopewa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt Samia Suluhu Hassan.

Amesema Rais Nyusi atawasili hapa nchini Kesho Jumatatu Julai 1,2024 ambapo atapokelewa na viongozi mbalimbali wa serikali katika uwanja wa ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere Jijini Dar Es Salaam na Kisha Julai 2 atakutana na Mwenyeji wake Rais wa Tanzania Ikulu Jijini Dar Es Salaam ambapo watafanya mazungumzo ya awali na baadaye Mkutano na waandishi wa Habari Kisha kufuatiwa na dhifa ya chakula Cha Mchana kilichoandaliwa na Rais Dkt Samia ambapo pia Julai 3 Rais Nyusi ndiye atakuwa mgeni rasmi katika Ufunguzi wa maonyesho ya sabasaba.

"Kama mnavyojua Msumbuji ni nchi rafiki Kwa Tanzania na Ina historia Kubwa nasi kwani hata chama Cha Frelimo chama kilichopigania Uhuru wa Msumbiji kilianzishwa hapa nchini na hata kiongozi wa chama hicho alifariki na kuzikwa Jijini Dar Es Kwa hiyo ziara hii ni muhimu sana kwani mahusiano yetu ni ya muda mrefu" amesema Makamba.

Makamba amesema ziara hiyo pia itaangazia katika masuala mengine muhimu ambapo pia Rais Filipe Nyusi na jopo lake na mwenyeji wake Rais Dkt Samia watasaini mikataba mbalimbali  ya ushirikiano ikiwemo katika masuala ya Habari,Afya na Elimu.

Kuhusu ushirikiano katika masuala ya ulinzi na usalama kati ya Tanzania na Msumbuji,Waziri Makamba amesema Tanzania imekuwa ni sehemu ya kuchagiza usalama katika Jimbo la Cabo Delgado lililo Kaskazini Mwa nchi hiyo ambapo Tanzania imechangia Kwa kupeleka Askari wake kwenye Jimbo hilo lenye migogogoro ya mara kwa mara ili kulinda usalama Jambo ambalo limerejesha Kwa kiasi kikubwa Hali ya usalama jimboni humo ambapo awali lilikuwa na hali tata ya kiusalama.

Hata hivyo waziri Makamba amesema ziara ya Rais huyo wa Jamhuri ya Msumbuji itakuwa ndiyo ziara ya mwisho ya Kiongozi huyo kama Mkuu wa nchi ambaye anatarajiwa Kumaliza muhula wake wa pili wa uongozi Oktoba mwaka huu.

"Kama mnavyojua waandishi wa Habari Rais Nyusi anategemea kumaliza utawala wake kama Rais wa Msumbuji baadaye mwaka huu ambapo nchi hiyo itafanya uchaguzi mkuu Oktoba 2024 hivyo itakuwa ni ziara yake ya mwisho kama Rais ya kuja kuwaaga watanzania na hata Mgombea urais wa Msumbuji kupitia chama tawala Cha Frelimo alifanya ziara hapa nchini kujitambulisha"ameongeza Makamba.

Rais Nyusi mara baada ya kuwasili hapa nchini kuzungumza na Rais Samia na hatimaye kufungua Maonyesho ya kimataifa ya biashara maarufu kama Sabasaba pia ataelekea visiwani Zanzibar Kwa ziara binafsi na baadaye ataondoka visiwani humo kurudi nchini mwake kupitia uwanja wa ndege wa Zanzibar wa Aman Abeid Karume Julai 4,2024.

Comments