MPINA AIBUA MASWALI KUHUSU DENI LA TAIFA, BEI YA MAFUTA NA MISAMAHA YA KODI KATIKA BAJETI YA 2026/27
MPINA AIBUA MASWALI KUHUSU DENI LA TAIFA, BEI YA MAFUTA NA MISAMAHA YA KODI KATIKA BAJETI YA 2026/27
Naibu Waziri Mkuu Kivuli na Waziri Kivuli wa Nishati na Madini, Luhaga Mpina, ameibua maswali mazito kuhusu mwelekeo wa Bajeti Kuu ya Serikali ya mwaka 2026/27, akidai kuwa bajeti hiyo imejaa ahadi zisizoendana na hali halisi ya uchumi wa wananchi na imepuuza changamoto muhimu zinazoikabili Tanzania.
Akichambua bajeti hiyo, Mpina alisema deni la taifa limeendelea kuongezeka kwa kasi na kufikia zaidi ya shilingi trilioni 53 katika kipindi cha miaka mitano iliyopita, huku wananchi wakikosa kuona miradi mikubwa ya maendeleo inayolingana na kiwango hicho cha ukopaji.
Alisema sehemu kubwa ya madeni hayo ni ya fedha za kigeni, hali ambayo inaweza kuongeza hatari kwa uchumi wa taifa endapo thamani ya shilingi itaendelea kushuka dhidi ya sarafu za kimataifa.
“Watanzania wanapaswa kuambiwa ukweli kuhusu mikopo inayochukuliwa na namna inavyotumika. Kuna mikopo mingi ambayo matumizi yake hayajulikani wazi kwa wananchi wala wabunge,” alisema Mpina.
Ahoji matumizi ya mikopo
Mpina alitaka serikali kuweka hadharani taarifa zote za mikopo na matumizi yake pamoja na kufanyika kwa ukaguzi maalum ili kubaini kama fedha hizo zilitumika kwa malengo yaliyokusudiwa.
Kwa mujibu wake, Tanzania haiwezi kujenga uchumi imara ikiwa sehemu kubwa ya mapato ya serikali itaendelea kuelekezwa kwenye ulipaji wa madeni badala ya huduma za msingi na maendeleo ya wananchi.
Bei ya mafuta yaendelea kuwa mzigo
Katika sekta ya nishati, Mpina alisema bajeti ya mwaka 2026/27 imeshindwa kutoa suluhisho la kudumu kwa tatizo la kupanda kwa bei za mafuta nchini.
Alidai kuwa pamoja na serikali kutangaza kutoa ruzuku ya kupunguza makali ya bei za mafuta, wananchi wengi hawajaona manufaa ya hatua hiyo kutokana na bei kuendelea kuwa juu.
Aidha, alieleza kuwa bei za mafuta katika soko la dunia zimekuwa zikishuka lakini hali hiyo haijaakisiwa kikamilifu katika soko la ndani, jambo linalozua maswali kuhusu mfumo wa ununuzi na usambazaji wa mafuta nchini.
Aitaka serikali kuchunguza zabuni za mafuta
Mpina alihoji uamuzi wa serikali kubadili mfumo wa ununuzi wa mafuta na kuhusisha kampuni za kati katika mchakato huo, akidai kuwa hatua hiyo imeongeza gharama badala ya kuzishusha.
Alisema kuna haja ya kufanya uchunguzi wa kina kuhusu mikataba na zabuni za mafuta ili kubaini kama taifa limepata thamani halisi ya fedha zake.
“Kama kuna watumishi au viongozi waliohusika katika maamuzi yaliyoisababishia nchi hasara, basi wawajibishwe,” alisema.



Comments