RAIS SAMIA MGENI RASMI TAMASHA LA TATU LA UTAMADUNI LA KITAIFA

 RAIS SAMIA MGENI RASMI TAMASHA LA TATU LA UTAMADUNI LA KITAIFA



Na. Marietta Kerenge - WUSM


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt Samia Suluhu Hassan anatarajiwa kuwa mgeni rasmi katika Tamasha la Tatu la Utamaduni ambalo litafanyika kwa siku nne kuanzia Septemba 20 hadi 23, 2024 wilayani Songea mkoani Ruvuma.


Akizungumza katika mkutano wake na Waandishi wa Habari jijini Dodoma leo Septemba 10, 2024, Katibu Mkuu Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo, Gerson Msigwa  amesema tamasha hilo linatokana na maelekezo ya Mhe. Rais Samia ya kufanyika kila mwaka katika mikoa mbalimbali ambapo kwa mara ya kwanza lilifanyika mwaka 2022 jijini Dar es Salaam na mwaka huu litafanyika mkoani Ruvuma na kufunguliwa na Waziri wa wizara hiyo, Mhe. Dkt. Damas Ndumbaro.


"Matamasha haya yamekuwa na manufaa mbalimbali kwenye jamii ikiwa ni pamoja na kuenzi utamaduni wetu, kuimarisha utangamano wa kitaifa, kuitangaza nchi, kutangaza vivutio vya kiutalii na kiutamaduni, fursa za kiuchumi, kiutamaduni na kijamii, pia kutanua wigo na mitandao ya kibiashara kwa bidhaa zinazozalishwa nchini hususani bidhaa za utamaduni, sanaa, na ubunifu". Amesema Msigwa.


Tamasha hilo lililobebwa na kaulimbiu ya “UTAMADUNI WETU NI UTU WETU, TUUEZI NA KUUENDELEZA”,  linatarajiwa kuwa na vitu tofauti na miaka mingine kutokana na maandalizi ya kipekee yakuvutia yaliyosheheni vitu vya kitamaduni.

Comments